Rais aipasua kichwa Ukawa 2015

Reported by: HENRY MWALWALA


Kutekeleza hilo, Jumapili iliyopita wenyeviti wa vyama hivyo, Profesa Ibrahimu Lipumba (CUF), Freeman Mbowe (Chadema), James Mbatia (NCCR- Mageuzi) na Dk Emmanuel Makaidi (NLD) walisaini makubaliano ya ushirikiano huo katika mkutano mkubwa wa hadhara uliofanyika Viwanja vya Jangwani.PICHA|MAKTABA 


Dar es Salaam. Baada ya vyama vinne vya upinzani nchini kusaini makubaliano ya kushirikiana pamoja na kusimamisha mgombea mmoja katika chaguzi zote zijazo, umoja huo sasa unakabiliwa na kazi ngumu ya kuweka sawa mambo, ikiwa ni pamoja na mchakato wa kumpata mgombea urais, kabla ya filimbi ya uchaguzi kupulizwa.
Vyama hivyo vitalazimika kufanya uamuzi katika sera tofauti za vyama vyao, kukabiliana na Sheria ya Uchaguzi, taratibu za kupata wagombea wa kuanzia ngazi ya chini hadi urais na jinsi ya kuendesha kampeni zao kabla ya kuwaendea wananchi kuwaeleza kuwa wameshajizatiti kukabiliana na chama tawala, ambacho kina mtandao karibu nchi mzima uliojengwa kwa miaka mingi.
Vyama hivyo vimeibuka na nguvu mpya baada ya kuunganishwa na hoja ya kutetea Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa na iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba ambayo ilielezewa kuwa ilitokana na maoni ya wananchi na hivyo kuunda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kupambana na wajumbe wa CCM kwenye Bunge Maalumu la Katiba.
Vyama hivyo, Chadema, CUF, NCCR Mageuzi na NLD vilisusia mchakato wa Katiba kwa kile vilichodai kuwa ni kutoridhishwa na mambo yalivyokuwa yakiendeshwa na sasa umoja wao umekwenda mbali zaidi kutaka kushirikiana kwenye chaguzi.
Kutekeleza hilo, Jumapili iliyopita wenyeviti wa vyama hivyo, Profesa Ibrahimu Lipumba (CUF), Freeman Mbowe (Chadema), James Mbatia (NCCR- Mageuzi) na Dk Emmanuel Makaidi (NLD) walisaini makubaliano ya ushirikiano huo katika mkutano mkubwa wa hadhara uliofanyika Viwanja vya Jangwani.
Moja ya kazi ngumu inayoukabili umoja huo ni jinsi ya kumpata mgombea wa urais atakayetoa upinzani mkubwa zaidi kwa mgombea wa chama tawala na kuendelea kupunguza kura za CCM baada ya mafanikio ya mwaka 2010 ya kupunguza asilimia 20 za kura alizopata RaisJakaya Kikwete mwaka 2005.
Kazi hiyo ngumu inatokana na tofauti za kisera baina ya vyama hivyo, wagombea urais wanaoonekana kuwa na sifa na matokeo ya uchaguzi uliopita uliompa mgombea wa Chadema, Dk Willibrod Slaa asilimia 26 ya kura zote na kuweka rekodi ya upinzani kukusanya kura nyingi.
Wakati Chadema ikitegemea mtaji wa Dk Slaa, ambaye ni katibu mkuu wa Chadema, wa asilimia 26.34 ya kura za mwaka 2010, CUF imekuwa ikimsimamisha mwenyekiti wake, Prof Lipumba katika chaguzi nne zilizopita, huku NCCR-Mageuzi ikiwa na mwenyekiti wake, james Mbatia na NLD ikiwa na Makaidi.
Mbowe alisema hilo halitakuwa tatizo kubwa katika kufikia uamuzi wa mgombea urais.
“Kwanza niseme tu kuwa hapa tulipofika haikuwa rahisi sana kama watu wanavyodhani, kwa hiyo yako mengi ambayo yamefanyika kwa kujadiliana na katika mchakato huu tumejifunza mengi. Kwa hiyo taratibu zitawekwa na zitafuatwa. Kutakuwa na vigezo na mambo kama hayo,” alisema mwenyekiti wa Chadema Freeman Mbowe alipozungumza na gazeti hili mwishoni mwa wiki akijaribu kuonyesha kuwa wamezingatia mambo mengi kabla ya kusaini makubaliano hayo.
“Suala la mgawanyo wa nafasi za kugombea haliwezi kutugombanisha. Ushindani si jambo geni kwetu maana tumekuwa na ushindani siyo sasa tu, bali hata ndani ya vyama. Hata katika chama kimoja huwa kuna wagombea zaidi ya mmoja.”
Kauli ya Mbowe iliungwa mkono na Mbunge wa Kigoma Kusini (NCCR-Mageuzi), David Kafulila ambaye alisema ili kuondoa utata wowote unaoweza kujitokeza, kamati ya ufundi itaundwa kwa ajili ya kushughulikia masuala yote muhimu.

Comments

UNITEC COMPUTER ACCESS