Skip to main content

Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete akutana na UKAWAK

25th August 2014

Rais Mstaafu Benjamin Mkapa
Wakati Rais Jakaya Kikwete akishinikizwa na makundi mbalimbali ya kijamii yakimtaka kusitisha kwa muda Bunge Maalum la Katiba, Rais Mstaafu Benjamin Mkapa, amejiweka mbali kabisa na Bunge hilo na mchakato wa Katiba, akiweka wazi kuwa hatazungumzia vitu hivyo.

Mkapa alisema hayo wakati wa kumkaribisha Waziri Mkuu Mizengo Pinda, katika hafla ya chakula cha jioni ya harambee ya Taasisi ya Benjamin William Mkapa Hiv/Aids (BMAF), mradi wa Mkapa Fellows, jijini Mwanza juzi.

“Sitaki kuzungumzia suala la Katiba Mpya wala mchakato wake unavyoenda,” alisema kwa kifupi Mkapa.

Ingawa Mkapa hakuwa ametakiwa kuzungumzia mchakato wa Katiba mpya wala Bunge Maalum la Katiba katika hafla hiyo, aliamua kuchomeka maneno hayo ya utangulizi pengine kujiweka mbali na mjadala wa katiba unaoendelea nchini kwa sasa.

Kadhalika halfa hiyo ambayo ilikuwa imejaa wanasiasa, akiwamo Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Uratibu na Uhusiano), Steven Wasira, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Tamisemi), Hawa Ghasia, Naibu Waziri wa Uchukuzi, Charles Tizeba na Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Steven Kebwe.

Wengine ni Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, ambaye pia anakaimu mkoa wa Mara, Everest Ndekiro, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Ali Rufunga, Mkuu wa Mkoa wa Geita, Magalula Ali Magalula, na wabunge wa CCM kutoka majimbo ya Kanda ya Ziwa.

Kutokana na uwapo wa wanasiasa hao, kulikuwa na hisia kwamba huenda Mkapa angezungumzia mchakato huo, kwani umekuwa ukitawala mijadala mingi ya wanasiasa kwa sasa nchini.

Bunge la Katiba limegawanyika tangu wabunge wanaounda Umoja wa Kutetea Katiba ya Wananchi (Ukawa) wajiengue na kuapa kutorejea huko kwa kile walichosema ni kuchakachuliwa kwa rasimu ya Katiba Mpya ambayo iliwasilishwa na Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba.

Ukawa unaoundwa na wabunge kutoka Chadema, CUF, NCCR-Mageuzi, NLD na DP, umekuwa ukiishutumu hotuba ya ufunguzi ya Bunge hilo ya Rais Kikwete kuwa ndiyo iliagiza kuchakachuliwa kwa rasimu hiyo.

Kutokana na kususia Bunge hilo, shinikizo limekuwa likielekezwa kwa Rais Kikwete alisitishe kwa madai kuwa kinachojadiliwa kwenye bunge hilo siyo Rasimu ya Katiba Mpya kama ilivyoandaliwa kutokana na maoni ya wananchi yaliyokusanywa na Tume ya Madiliko ya Katiba.

Hata hivyo, wiki iliyopita Kamati Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), ilikutana mjini Dodoma na kuridhia Bunge la Katiba kuendelea na mchakato wa kujadili rasimu hiyo.

Bunge Maalum la Katiba linaloendelea mjini Dodoma kwa sasa linaelezwa kugubikwa na wajumbe kutoka CCM na wanafanya mabadiliko makubwa ya Rasimu ya Katiba ili kukidhi matakwa yao ya kisiasa.

Miongoni mwa mambo ambayo yameleta kutokuelewa kwingi ni mabadiliko ya kuondoa mfumo wa Muungano wa serikali tatu unaopendekezwa na Rasimu ya Katiba Mpya na badala yake kuingiza serikali mbili.

Ukawa wamekwisha kuweka wazi kuwa watafanya maandamano na mikutano mikubwa nchi nzima kuhamasisha wananchi waikatae katiba itakayotolewa na Bunge hilo kwa kuwa ni batili.

MKAPA FELLOWS NA AFYA
Baada ya utambulisho huo, Mkapa alisema taasisi hiyo iliyoanzishwa 2006 imekuwa mstari wa mbele kuchangia juhudi za serikali kupitia miradi mbalimbali inayolenga kuimarisha huduma za afya.

Alisema taasisi hiyo iliyoanzishwa kutokana na ushauri wa Rais wa zamani wa Marekani, Bill Clinton, imesaidiana na serikali na wala si kushindana katika kutoa huduma za afya hususani vijijini.

“Vijana wa taasisi hii wamefanya kazi nzuri kwani wameenda kufanya kazi kule ambako watumishi wa serikali walikuwa hawataki kwenda…tumeshirikiana vizuri na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii,” alisema Mkapa.

Mkapa alisema mradi mmojawapo unaotekelezwa na taasisi hiyo ni “Mkapa Fellows” ukiwa ni wa miaka mitano (2013/17) katika halmashauri 15 za mikoa ya Shinyanga, Kagera, Simiyu, Rukwa na Zanzibar.

AJIRA 156
Awali Ofisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi hiyo, Dk. Ellen Mkondya-Senkoro, alisema ofisi yao imeajiri watumishi 156 kwa ajili ya kufanyakazi katika vituo vya tiba mikoa ya Kanda ya Ziwa.

“Kutokana na kuajiri watumishi hawa, pia tunatarajia kujenga vyumba vya upasuaji 23 na wodi ya wajawazito ngazi ya vituo vya afya utakaoanza Januari mwakani,” alisema Dk. Senkoro.

Alisema lengo la mradi huo kwa miaka mitano ni kuajiri wataalamu wa afya 180,  kujenga uwezo wa wataalam wa afya katika masuala ya Ukimwi na utoaji wa elimu kwa jamii.

Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa BMAF, Balozi Charles Sanga, alisema mradi wa Mkapa Fellows umefikia karibu asilimia 80 ya maeneo nchini na kufanikisha mengi.

Alisema yaliyofanikishwa ni pamoja na utoaji wa ajira kwa wataalam wa afya 1000 vijijini, ufadhili wa wanafunzi 700 wa kada ya afya na ujenzi wa nyumba 310 za wafanyakazi wa afya katika wilaya 31.

PINDA APONGEZA
Pinda  katika hafla hiyo alimshukuru na kumpongeza Mkapa kwa kuanzisha taasisi hiyo ambayo inachangia jitihada za serikali kuimarisha huduma za afya.

Alisema kazi nzuri inayofanywa na taasisi hiyo katika mikoa ya Kanda ya Ziwa na sehemu nyingine, inaungwa mkono na serikali moja kwa moja.
“Lengo la mradi huu ni kuimarisha huduma za afya hasa mapambano dhidi ya Ukimwi na kuimarisha afya ya mama na mtoto kupitia uimarishaji wa rasilimali watu katika sekta ya afya hususani maeneo yenye mazingira magumu,” alisema Pinda.

Aidha, alisema hafla ya uchangiaji wa mfuko huo unaotegemewa kugharimu Sh. bilioni 15 kwa miaka mitano, tayari umefanikisha kukusanya Sh. bilioni 4.9 mpaka sasa.

Katika harambee hiyo iliyokuwa na malengo ya kukusanya Sh. 500,000,000 ilifanikisha kupatikana kwa Sh. bilioni 1.383 zikiwa ni pesa taslimu na ahadi.

Wakati huo huo, juzi asubuhi Waziri Mkuu alitembelea na kukagua ujenzi wa uwanja wa ndege wa kisasa jijini Mwanza pamoja na kutembelea ujenzi wa jengo la kimataifa la biashara linalojengwa kati ya makutano ya Makongoro na Furahisha.

Comments